Na: Nassoro Rashid – Mkinga, Tanga
Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Mkinga, Ndugu Juma Jackson Hamadi, amefungua rasmi mafunzo ya siku moja kwa Makarani Waongozaji Wapiga Kura, akisisitiza umuhimu wa uadilifu, uzingatiaji wa sheria, na uwajibikaji wa hali ya juu katika utekelezaji wa majukumu yao kuelekea Uchaguzi Mkuu Oktoba 29, 2025.
Akizungumza katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mkinga, Hamadi alisema mafunzo hayo ni sehemu muhimu ya maandalizi ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) katika kuhakikisha kuwa uchaguzi unakuwa huru, wa haki, wenye uwazi na amani.
“Dhamana mliyopewa ni kubwa na nyeti. Mnapaswa kutekeleza majukumu yenu kwa kuzingatia Katiba, Sheria, Kanuni na maelekezo ya Tume. Huu si wakati wa majaribio, bali ni wakati wa kufanya kazi kwa uadilifu na uaminifu,” alisema Hamadi.

Alifafanua kuwa jumla ya makarani waongozaji 339 wanashiriki mafunzo hayo, ambapo watasambazwa katika vituo 295 vilivyopo katika kata 22 za Wilaya ya Mkinga. Watendaji hao, alisema, ndio watakaokuwa kiungo muhimu kati ya Tume na wananchi siku ya kupiga kura.
“Ninyi ndio mnakutana ana kwa ana na wapiga kura, hivyo hakikisheni mnatenda kwa unadhifu, lugha nzuri, na kutoa huduma bora kwa kila mpiga kura bila upendeleo. Wapeni kipaumbele wapiga kura wenye mahitaji maalum,”. Alisema Ndugu Hamadi.
“Tangu siku ya uteuzi wenu, ninyi ni watumishi wa Tume. Simamieni viapo vyenu, mtunze siri za uchaguzi na fanyeni kazi kwa maslahi ya Taifa letu,” alisisitiza
Kwa upande wake, Mwezeshaji wa Mafunzo, Ndugu Rajabu Mangala, alisema mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa kwani yanawapa makarani uelewa wa kina kuhusu utaratibu wa upigaji kura, uhesabuji wa kura na utunzaji wa nyaraka za uchaguzi. Alisisitiza kuwa uelewa huo utasaidia kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa utulivu, uwazi na ufanisi mkubwa.
Naye, Bi. Mwanaidi Jumaa Mashango, akizungumza kwa niaba ya makarani wenzake, alisema wamepokea vyema mafunzo na maelekezo waliyopewa, na wako tayari kutekeleza majukumu yao kwa weledi na uaminifu mkubwa.
“Tumejifunza kwa kina majukumu yetu na tunakwenda kufanya kazi kwa uadilifu, tukizingatia sheria na maelekezo yote tuliyopewa. Tutaenda kutumikia Taifa kwa uaminifu na bidii,” alisema Bi. Mwanaidi.
Hamadi aliongeza kuwa kwa kipindi chote cha uchaguzi, watendaji hao wanawajibika moja kwa moja kwa Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) na si mamlaka nyingine yoyote.

Kasera, Tanga -HorohoroRoad
Postal Address: P O Box 6005 Tanga
Simu: +255 027-2660501
Simu: +255 684 625 299
Barua Pepe: Info@mkingadc.go.tz
Mkinga dc @ 2017