"BILA UMOJA NA MSHIKAMANO HATUTAWEZA KUITENDEA HAKI IMANI TULIYOPEWA NA WANANCHI" - MHE. GILBERT KALIMA
Na: Nassoro Rashid - Mkinga
Desemba 3, 2025
Mkuu wa Wilaya ya Mkinga, Mhe. Gilbert Kalima, ametoa wito mzito kwa Baraza Jipya la Madiwani kuhakikisha umoja, ushirikiano na mshikamano vinakuwa nguzo kuu ya utekelezaji wa majukumu yao katika kipindi kipya cha uongozi.
Akihutubia katika Mkutano wa Kwanza wa Baraza la Madiwani, Mhe. Kalima amesema kuwa bila kuungana na kufanya kazi kwa pamoja, viongozi hawataweza kuitendea haki imani kubwa waliyopewa na wananchi.
Ameonya kuwa endapo kutakuwepo mgawanyiko ndani ya Baraza, mambo muhimu ya maendeleo hayatapitishwa na hatimaye matarajio ya wananchi yatadumaa.
“Bila umoja na mshikamano, tutakuwa na mabaraza mawili au matatu ndani ya kikao kimoja. Tutapinga wenyewe kwa wenyewe na hatutafikia malengo wanayotamani wananchi wetu,” amesema.
Aidha, Mhe. Kalima amesisitiza umuhimu wa madiwani kuendeleza mafanikio makubwa ya halmashauri katika kuongeza mapato ya ndani. Amekumbusha kuwa mwaka 2020 Halmashauri ya Mkinga ilikuwa inakusanya milioni 800 pekee, lakini kwa nguvu ya pamoja, mapato hayo yamefikia takribani shilingi bilioni 3 katika mwaka uliopita wa fedha.
Amesema kuendelea kupanda kwa mapato kutategemea kiwango cha ushirikiano baina ya madiwani, watendaji na viongozi wa kisiasa.
“Tukikosa mshikamano tutarudi nyuma. Kwani bila ya umoja na mshikamano hatutaweza kuitendea haki imani tuliyopewa na wananchi, Hii tusiruhusu kamwe,” amesisitiza
Sanjari Mkuu huyo wa wilaya ametoa pongezi kwa Mkurugenzi Mtendaji, Watendaji na Idara zote kwa kuendelea kuihudumia Mkinga kwa umahiri katika kipindi chote ambacho Baraza la Madiwani lilikuwa limevunjwa.
Amesema taarifa walizowasilisha mbele ya baraza ni ushahidi wa kazi kubwa na ya mfano inayofanywa na watumishi wa Halmashauri.
Akigusia fedha zinazotolewa na serikali kuu, ikiwemo milioni 800 kwa uendelezaji wa Hospitali ya Wilaya, Mhe. Kalima amesisitiza kuwa jukumu la madiwani sasa ni kufuatilia na kusimamia matumizi ya fedha hizo kwa mujibu wa malengo yaliyokusudiwa.
“Fedha hizi zikitumika sawa, tutakuwa tumewatendea haki wananchi. Tusipokuwa wamoja tutaathiri usimamizi wake,” amesema.
Pia Mkuu wa Wilaya amesisitiza kuwa amani na utulivu ndivyo vinavyofanya shughuli zote za maendeleo ziendelee. Ameitaka jamii na viongozi wote kuwa walinzi wa amani, akisema bila utulivu hakuna uwezekano wa kuboresha huduma za jamii kama maji, afya, elimu na barabara.
“Amani ndio msingi wa maendeleo yote. Tuihifadhi, tuilinde na tuihubiri kwa nguvu zote,” amesema.
Mhe. Kalima ametamatisha kwa kuwataka viongozi wote wa Mkinga kutanguliza maslahi ya wananchi na kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na moyo wa kujitoa kwani umoja wa viongozi ndio shukrani ya kweli wanayoweza kuirudisha kwa wananchi waliowachagua.

Kasera, Tanga -HorohoroRoad
Postal Address: P O Box 6005 Tanga
Simu: +255 027-2660501
Simu: +255 684 625 299
Barua Pepe: Info@mkingadc.go.tz
Mkinga dc @ 2017